Ujauzito Wiki ya 5

Jinsi mtoto wako anavyokua katika ujauzito wiki ya tano
Ingawa bado huonekani mjamzito, ndani ya mwili wako mtoto anakua kwa kasi. Japokuwa ni kiinitete (embryo), mtoto wako bado anaonekana zaidi kama kiluwiluwi kuliko mwanadamu. Viungo vyake vikuu vinajengeka, figo na moyo wa mtoto wako vinakua, na mirija ya nyuroni (neural tube) ambayo inalinda uti wa mgongo na kuunganisha ubongo wake inajifunga.

Dalili za ujauzito katika wiki ya tano
Ingawa baadhi ya wanawake hawahisi ni wajawazito katika wiki ya tano, unaweza kuanza kuhisi dalili hizi.
Unaweza kujikuta ukikinai au kuchefukwa na baadhi ya vyakula na kupelekea kutapika. Hii hutokea kwa idadi kubwa ya wajawazito katika kipindi cha miezi mitatu ya mwanzo.

Unapojisikia kuchoka au kuzidiwa na uchovu na kupelekea kulala ghafla, hii ni hali ya kawaida kabisa kwa wajawazito hasa miezi mitatu ya mwanzo.
Ujauzito husababisha kufurika kwa homoni mwilini, hii husababisha matiti kuuma, kusikia kwenda haja ndogo mara kwa mara na kichwa kuuma. Zifahamu njia mbadala za kukabili maumivu ya kichwa bila kutumia dawa za hospitali.

Ingawa dalili hizi zinakera, jua hazitakaa milele. Fahamu zaidi kuhusu namna unavyoweza kujisikia katika miezi mitatu ya mwanzo ya ujauzito kwenye mjumuisho wetu wa taarifa za mwanzoni mwa ujauzito.

Unachotakiwa kufahamu katika ujauzito wiki ya tano
Jaribu kujenga tabia ya kula vizuri. Unahitaji kuweka viwango vya juu vya nishati yako, na mtoto wako atafaidika kama vyakula unavyokula vina virutubisho mbalimbali.
Kula kiasi kidogo cha chakula na kinywaji mara kwa mara huweza kusaidia mmeng’enyo wa chakula na kupunguza kichefuchefu.

Jipatie vitamini C kwa wingi kila siku, hasa hasa kwenye kipindi hichi ambacho seli za mtoto wako zinakua kwa kasi sana. Vyanzo vizuri vya vitamini C ni pamoja na: machungwa, pilipili hoho nyekundu, n.k. Unatakiwa uwe umeshaanza kutumia virutubisho vya foliki aside na vitamini D, lakini ni vyema ukatambua kama ni wazo zuri kutumia virutubisho zaidi.
Kama una kazi anza kufikiria kuhusu likizo ya uzazi na kama kuna malipo ambayo unatakiwa upewe. Wasiliana na daktari kuhusu ni lini unaweza kuana kuhudhuria kliniki ya uzazi.

Programu ya AfyaTrack

Programu ya kwanza nchini Tanzania ya kufuatilia maendeleo ya ujauzito na ukuaji wa mtoto kwa lugha ya Kiswahili.