Ujauzito Wiki ya 4

Jinsi mtoto wako anavyokua katika ujauzito wiki ya nne
Ndani ya mwili wako, ukuaji wa kushangaza unaendelea. Mviringo wa seli unaogawanyika ndani ya mfuko wako wa uzazi tayari umeshakuwa kiinitete (embryo). Ukubwa wake kwa sasa ni sawa na ukubwa wa punje ya ulezi. Wiki tano zijazo ni muhimu sana kwa ukuaji wa mtoto wako. Kirutubishi mimba (Placenta) na Kiunganishi (umbilical cord) kinacholeta virutubisho na oksijeni kwa mtoto wako, tayari vimeshaanza kufanya kazi.

Dalili za ujauzito kwenye wiki ya nne
Wiki hii ndio inaweza ikawa mara yako ya kwanza kujisikia kabisa kuwa ni mjamzito. Moja ya dalili za mwanzo kuwa ni mjamzito ni matiti kuuma ukiyagusa au kuyabonyeza.
Pia unaweza kuanza kupata kutoka damu kwa mbali sana au vitone vidogo vidogo vinavyoweka vidoa vidogo tuu kwenye nguo yako ya ndani kipindi kile ambacho ungetegemea kupata siku zako za hedhi kwa kawaida. Hii ni kawaida kabisa, ila ni vizuri kuhakikisha kila unapotokwa na damu ukiwa mjamzito kumuona daktari.

Je umeanza kujisikia kichefuchefu? Inawezekana unakumbana na hali ambayo ni maarufu sana kwa wanawake wajawazito, kichefuchefu kikali kipindi cha asubuhi (morning sickness). Baadhi ya wanawake wajawazito huwa na kutapika sana (Hyperemesis gravidarum), ugonjwa ambao unasababisha chochote wanachokula kukaa tumboni na ni lazima wakitapike. Kama hii itakutokea tafadhali muone daktari mara moja.

Unachotakiwa kufahamu katika ujauzito wiki ya nne
Kama kipimo cha ujauzito kilionyesha hauna ujauzito au kilishindwa kutoa majibu sahihi, na bado haujaziona siku zako za hedhi mpaka sasa, unaweza ukarudia tena kipimo muda huu.
Ikiwa kipimo kimeonesha una ujauzito au la, sasa ni wakati wa kuanza kutumia virutubisho vya folic acid, kama bado ulikuwa haujaanza kutumia bado. Virutubisho vya foliki asidi vinasaidia kumkinga mtoto wako asipate matatizo ya uti wa mgongo na ubongo (neural tube defects), kwa mfano spina bifida. Meza kidonge kimoja cha foliki asidi cha 400mcg kwa siku.

Kama Kizio cha ukubwa wa mwili kwa uzito wako (Body mass index – BMI) ni Zaidi ya 30, muone daktari kwani atahitaji kuongeza dozi ya foliki asidi unayotakiwa kutumia.
Itakushangaza kutambua ya kwamba huu ndio wakati muafaka kuanza utaratibu wa kufanya mazoezi mepesi. Mazoezi yatakufanya utengeneze misuli yenye nguvu na uvumilivu.

Ni kawaida kiafya kuongezeka uzito wakati wa ujauzito, na mazoezi yatakusaidia kusimamia kuongezeka kwa uzito. Kama uzito wako upo juu kiasi (overweight), kufuata utaratibu mzuri wa mazoezi utakufanya usiongezeke zaidi.
Inashangaza kutambua lakini ni ukweli kwamba mazoezi pia yanasaidia kuwa thabiti kipindi cha uchungu. Ukifikia kipindi cha uchungu, utashukuru kutumia muda wako kufanya mazoezi mara kwa mara. Chagua mazoezi mepesi na ambayo unapenda kufanya: kutembea na kuogelea ni mojawapo ya mazoezi ambayo ni salama kipindi cha ujauzito.

Programu ya AfyaTrack

Programu ya kwanza nchini Tanzania ya kufuatilia maendeleo ya ujauzito na ukuaji wa mtoto kwa lugha ya Kiswahili.