Kunyonyesha Ukiwa Mjamzito

Je, ni Sawa Kuendelea Kunyonyesha Mtoto Wakati una Mimba Nyingine?

Kunyonyesha kunasaidia kuzuia kupata ujauzito, lakini sio mara zote. Inategemea na vitu kama vile mara ngapi unanyonyesha mwanao na umri wa mtoto wako. Kumbuka, inawezekana kushika mimba tena huku unanyonyesha mtoto wako.

Ikiwa utagundua wewe ni mjamzito tena, iwe ulipanga au bila kupanga, utakuwa na maswali mengi- kama kuendelea kumnyonyesha mtoto kutaathiri ujauzito wako mpya, mtoto anayenyonya, utokaji wa maziwa na mwili wako.

Ikiwa mama akagundua kuwa ni mjamzito wakati bado ananyonyesha. Mtoto anayenyonyeshwa anaweza kuwa mdogo hajafikia umri wa kuachishwa au mama mwenyewe anakuwa bado anapenda kumnyonyesha mtoto wake. Ikiwa mimba ni ya kawaida na yenye afya, inapendekezwa kuwa ni salama kabisa kuendelea kunyonyesha katika kipindi chote cha ujauzito. Katika makala hii utajifunza mambo muhimu na mikakati thabiti unayotakiwa kujua kuhusu unyonyeshaji ukiwa mjamzito.

Je, Nimuachishe Mtoto Kunyonya Mara Baada ya Kugundua Nina Ujauzito Mwingine?

Ujauzito mpya ni sababu iliyozoeleka ya kumuachisha mtoto kunyonya. Baadhi ya watoto wanaacha wenyewe na baadhi ya kina mama wanawahamasisha watoto wao kuacha kunyonya ili kujiandaa kwa ujio wa mtoto mpya atakayezaliwa. Lakini ikumbukwe hakuna haja ya kumuachisha mtoto kwasababu umeshika ujauzito mwingine. Unaweza kuendelea kumnyonyesha. Unaweza pia kuamua kuwanyonyesha wote wawili- mtoto mkubwa na kichanga wako atakayezaliwa.

Usalama wa Kunyonyesha Wakati wa Ujauzito

Kama umegundua umeshika ujauzito mwingine, hakikisha unaongea na mkunga au daktari wako juu ya historia ya afya yako. Daktari atakusaidia kufanya maamuzi sahihi kuhusu kuendelea kunyonyesha au kumuachisha mwanao.

Kawaida kunyonyesha baada ya kugundua una ujauzito mpya ni salama kabisa. Ikiwa una afya nzuri na ujauzito wako hausababishi matatizo yeyote ya kiafya, unaweza kuendelea kunyonyesa. Ingawa, zipo baadhi ya hali daktari akizishuhudia katika afya yako atakushauri umwachishe mwano kunyonya.

Wakati unanyonyesha mwili wako unatoa kichocheo kinachoitwa “oxytocin”. Homoni hii inawaunganisha mtoto na mama na kuleta upendo, vilevile homoni hii inasababisha mibano na mikazo ya mfuko wa uzazi (uterasi). Mibano na mikazo (The Braxton Hicks Contractions) hii sio hatari kwa ujauzito wa kawaida na wenye afya.

Sababu Ambazo Daktari Atakushauri Umuachishe Mtoto Kunyonya

Daktari anaweza kuwa na wasiwasi na kukushauri umwachishe mtoto kunyonya kama:

  • Ujauzito wako uko katika hatari kubwa ya kutoka
  • Ulishapitia tatizo la mimba changa kuharibika au kutoka
  • Ulijifungua kabla ya mda katika ujauzito uliopita (kabla ya wiki ya 37)
  • Unapata maumivu ya tumbo yanayoambatana na kutoka damu ukeni
  • Una ujauzito wa mapacha au zaidi
  • Hauongezeki uzito sahihi wenye afya.

Je, Kunyonyesha Kunaweza Athiri Mtoto Aliye Tumboni?

Hakuna ushahidi kuwa kunyonyesha ukiwa mjamzito kutaumiza ujauzito wako mpya au kuingilia ukuaji na maendeleo ya mtoto anayekuwa tumboni. Mwili wako unaweza kutengeneza maziwa ya mtoto anaye endelea kunyonya huku ukimtoa virutubisho vyote anavyohitaji mtoto aliye tumboni. Vifuatavyo vidokezo muhimu unavyotakiwa kukumbuka:

  • Mwili wako unahitaji nishati ya kutosha ili kutengeneza maziwa, kutoa virutubisho muhimu kwaajili ya mtoto anayekua tumboni, na kukuweka mwenye afya na imara. Ili mwili wako kuwa na nguvu na kuepusha upungufu wa aina yeyote ya virutubisho muhimu, kunywa maji ya kutosha, kula mlo kamili ulio na nyongeza ya kalori zenye afya, na pata mapumziko ya ziada.
  • Ongea na daktari wako ikiwa una tatizo lolote la kiafya kama vile kisukari au anemia, ili kuhakikisha unapata virutubisho muhimu na kalori sahihi unazohitaji.
  • Hudhuria miadi yako kila mwezi na fanya uchunguzi mara kwa mara kila unapoweza, ni muhimu ili kuwa na uhakika kuwa ujauzito wako unaendelea vizuri na unaongezeka uzito kama inavyotakiwa.

Je, Ujauzito Wako Mpya Unaweza Kumuathiri Mtoto Anayenyonya?

Mabadiliko katika ladha ya maziwa na kupungua kwa kiwango cha maziwa huweza kumuathiri mtoto anayenyonya. Mambo haya mawili yanaweza kusababisha mtoto mwenyewe kukataa kunyonya. Ikiwa mtoto wako yuko chini ya mwaka mmoja, mabadiliko haya yaangaliwe kwa umakini zaidi ili kuhakikisha mtoto anapata virutubisho vya kutosha. Endelea kumnyonyesha ili asikose virutubisho muhimu kutoka kwenye maziwa ya mama. Lakini, ikiwa mtoto wako ni mkubwa na tayari kaanza kula vyakula vigumu na kula mwenyewe, mabadiliko ya ladha na kiwango cha maziwa hayawezi kumuathiri.

Mabadiliko ya ladha ya maziwa

Wakati mtoto wako amezaliwa, atapokea maziwa ya kwanza yanayoitwa “colostrum”. Kadiri ujauzito wako unavyoendelea kukua ndivyo ladha ya maziwa itakavyobadilika kuelekea kwenye “colostrum” kwaajili ya ujio wa mtoto mpya. Mambo machache unayotakiwa kujua kuhusu mabadiliko haya ni kuwa:

  • “Colostrum” imejaa kingamwili na virutubisho, hivyo ni nzuri kwa mtoto mkubwa anayenyonya. Lakini, mwili hautengenezi “colostrum” nyingi hakikisha kichanga wako anapata kwa wingi maziwa haya yenye kingamwili na virutubisho vya kutosha haswa kama utaamua kunyonyesha mtoto mkubwa na kichanga wako baada ya kujifungua.
  • Mtoto anaweza kuendelea kunyonya bila tatizo hata baada ya mabadiliko ya ladha ya maziwa, au anaweza asipende utofauti wa ladha na kuacha mwenyewe kunyonya.
  • Maziwa haya ya awali “colostrum” yanamsaidia mtoto mchanga kutoa kinyesi cha kwanza nje ya miili yao “meconium”, vilevile kwa mtoto mkubwa ambaye bado ananyonya anaweza kupata dalili za kuharisha kutokana na maziwa haya ya awali yaliyojaa virutubisho na kingamwili za kutosha.

Mabadiliko ya kiwango cha maziwa

Ujauzito ni moja ya sababu ya upungufu wa kiwango cha maziwa. Mambo machache unayotakiwa kujua ni kwamba:

  • Unaweza kuona kupungua kwa kiwango cha maziwa mara baada ya kushika ujauzito au baadae kidogo.
  • Ikiwa mtoto wako anayenyonya yuko chini ya mwaka mmoja na umegundua upungufu wa kiwango cha maziwa ongea na mkunga wako. Inaweza kukuhitaji kutumia maziwa ya fomula sambamba na kunyonyesha ili kuhakikisha mtoto anapata virutubisho anavyohitaji.
  • Kama mtoto wako ana umri zaidi ya mwaka mmoja, hakikisha anapata virutubisho anavyohitaji kutoka kwenye vyakula mbalimbali vigumu anavyokula. Unaweza kuendelea kumnyonyesha kama afya yako inaruhusu na mwanao yuko tayari kunyonya.
  • Upungufu wa kiwango cha maziwa unasababisha maziwa kutoka taratibu kwenye titi. Baadhi ya watoto wanakatishwa tamaa na hali hii na kuacha kunyonya wenyewe.

Je, Ujauzito Mpya Unaweza Kumuathiri Mama Anayenyonyesha?

Ingawa inawezekana kuendelea kunyonyesha wakati wa ujauzito, zipo changamoto. Zipo njia nyingi ambazo ujauzito unaweza kukuathiri kama mama anayenyonyesha. Zifuatazo ni baadhi ya changamoto unazoweza kupitia wakati wa kunyonyesha na vidokezo vitakavyokusaidia kukabiliana na changamoto hizo.

Kuvimba kwa matiti na chuchu.

Ujauzito unaweza kurejesha tatizo la kunyonyesha la zamani. Mabadiliko ya homoni yanayotokea wakati wa ujauzito yanaweza kusababisha tena maumivu ya chuchu na matiti. Kunyonyesha huku chuchu zimevimba kunaweza kuwa kugumu au kusababisha maumivu. Kwa bahati mbaya, suluhisho la chuchu zilizovimba wakati wa kunyonyesha halifanyi kazi wakati wa awali wa ujauzito kwasababu chanzo cha chuchu kuvimba ni mabadaliko ya vichocheo. Suluhisho la hali hii ni kuwa mvumilivu. Hali hii itadumu kwa miezi mitatu ya kwanza, japo kwa baadhi ya kina mama hali hii inaweza kuendelea kipindi chote cha ujauzito.

Unaweza kufanya yafuatayo ili kukabiliana na hali hii:

  • Weka kitu cha baridi juu ya chuchu zako
  • Vaa sidiria inayokufanya uwe huru (isikubane sana)
  • Jitahidi kumnyonyesha mtoto katika mazingira matulivu yatakayomfanya mtoto apunguze kuhangaika ili asisababishe kuvuta chuchu. Badala ya kumnyonyeshea sebuleni ambapo anaweza kubabaishwa na kelele za luninga au ndugu zake, nenda chumbani ambapo hakuna kelele au watu.
  • Jaribu mikao tofauti ya kunyonyesha.

Kuchoka

Ni kawaida kusikia uchovu kuliko kawaida ukiwa mjamzito kwasababu ya mabadiliko yote ya homoni yanayoendelea katika mwili wako. Kumlea mtoto mwingine na kumnyonyesha inaongezea uchovu huo. Kama unaweza, pata mapumziko ya kutosha. Inaweza kuwa ngumu haswa kama una mtoto anayetambaa au kukimbia kimbia, lakini fanya jitihada ya:

  • Kulala wakati mwanao akilala
  • Kaa kitako au lala kisha nyoosha miguu yako juu ukiwa unanyonyesha
  • Usiruke milo na kumbuka kunywa maji ya kutosha

Kadiri ujauzito unavyoendelea kukua, inakuwa ngumu kupata mkao mzuri wa kunyonyeshea mtoto wako. Fanya majaribio na tafuta mkao mpya utakaokupa unafuu wewe na mwanao. Pia unaweza kunyonyesha ukiwa umelala kwa ubavu.

Kumbuka

Wanawake wengi wanacha kunyonyesha mara baada ya kugundua wameshika ujauzito mwingine. Ikiwa hauko tayari, na daktari wako amekuhakikishia hakuna tatizo la kiafya linalokukabili hauna haja ya kumuachisha mwanao. Unaweza kuendelea kumnyonyesha mtoto wako kipindi chote cha ujauzito kwa usalama. Unaweza pia kuendelea kunyonyesha mwanao mkubwa hata baada ya kichanga wako kuzaliwa. Inaitwa “tandem nursing” kwa lugha ya kigeni.

Ni kweli, ujauzito unaleta kuvimba na maumivu ya matiti, kupungua kwa kiwango cha maziwa na uhitaji wa nishati ya zaidi mwilini. Ni rahisi kuchoka na kuelemewa. Unaweza kuamua kumuachisha mtoto wako kunyonya, na hii ni sawa kabisa. Ikumbukwe pia kuwa kipindi cha ujauzito kumuachisha mtoto kunyonya ni rahisi zaidi kwasababu ya mabadiliko ya ladha na kiwango cha maziwa, hivyo unaweza kuamua ni mda mzuri wa kuacha kunyonyesha. Fanya kile ambacho ni sahihi kwako na familia yako na usisikie hatia juu ya hilo.

IMEPITIWA: SEPTEMBA, 2021.

Programu ya AfyaTrack

Programu ya kwanza nchini Tanzania ya kufuatilia maendeleo ya ujauzito na ukuaji wa mtoto kwa lugha ya Kiswahili.